RAIS SAMIA AMEWEKA ALAMA ISIYOFUTIKA KWA WAFANYAKAZI WA TANZANIA, ARUDISHA NYONGEZA YA MISHAHARA KILA MWAKA.

 RAIS SAMIA AMEWEKA ALAMA ISIYOFUTIKA KWA WAFANYAKAZI WA TANZANIA, ARUDISHA NYONGEZA YA MISHAHARA KILA MWAKA.


Na Bwanku M Bwanku.


Leo Jumatatu Mei Mosi, ni maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani ambapo kitaifa hapa Tanzania yalifanyika mkoani Morogoro ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan alikuwa mgeni rasmi kwenye sherehe hizo za Wafanyakazi.


Wafanyakazi ni kundi muhimu sana kwenye ustawi wa Taifa lolote duniani na ndiyo hawa wanaotoa huduma na kutekeleza sera za uchumi na maendeleo ya Taifa. 


Rais Samia amelipa jicho la kipekee kundi hili muhimu kwa Taifa kwa kuangalia changamoto zao na yale wanayohitaji kuboreshewa ili wafanye kazi yao kwa weledi zaidi.


Leo kwenye sherehe hizo za Wafanyakazi, Rais Samia ametangaza uamuzi mkubwa wa Serikali yake katika kuboresha zaidi maslahi ya Wafanyakazi.


Rais Samia ametangaza kurudisha utaratibu wa nyongeza za mishahara kila mwaka kwa Wafanyakazi. Rais amesema kuna nyongeza za mishahara za kila mwaka ambazo zilisitishwa kwa muda, lakini mwaka huu Serikali yake imeona zirudi, nyongeza hizo za kila mwaka na zitaanza mwaka huu na zitaendelea kila mwaka.


Haya ni machache katika mengine ambayo Rais Samia anazidi kuweka alama kwa Wafanyakazi wa nchi hii tena mengine yaliyolalamikiwa kwa muda mrefu sana. 


Miaka miwili ya Rais Samia, baada ya kupita takribani miaka 6, Serikali ya Rais Samia imekata kiu ya Wafanyakazi wa Tanzania kwa kuongeza mishahara kwa asilimia 23.3. Nyongeza ya mishahara ni takwa la kisheria lililosubiliwa kwa hamu kubwa sana na kwa muda mrefu sana na Watumishi wa Taifa hili.


Kuingia kwa Rais Samia Suluhu Hassan madarakani kulifungua ukurasa mpya wa kukata kiu hii ya Wafanyakazi ambapo Mei Mosi Mwaka 2021 kwenye Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) pale Jijini Mwanza, Rais Samia aliwaahidi Wafanyakazi kwamba Serikali inakuja na package nzuri ya nyongeza ya mishahara baada ya uchumi kuimarika hasa baada ya Taifa kuwa kwenye mdororo mkubwa wa Kiuchumi uliotokana na mlipuko wa ugonjwa wa Corona. 


Hatimaye Mei Mosi ya Mwaka 2022 pale Dodoma, Rais Samia aliwaeleza Wafanyakazi kwamba jambo lao lipo( kuwaongezea mishahara) na kwamba Serikali yake inaliweka sawa kuangalia liwe kwa kiasi gani kwa kuzingatia Pato la Taifa (GDP), mapato ya ndani yanayotarajiwa kukusanywa kwa mwaka wa Fedha 2022/23 na hali ya Uchumi wa ndani na Nje ya Nchi. Sasa mishahara baada ya miaka 6 imeongezwa kwa asilimia 23.3.


Baada ya miaka kwa miaka ya kiu hii ya Wafanyakazi hatimaye mwishoni mwa wiki, Jumamosi Mei 14, 2022, Serikali ya Rais Samia ilitoa taarifa iliyolisimamisha Taifa na kulipua shangwe la furaha kila kona, taarifa ya Serikali kukubali na kuridhia kuongeza mishahara ya Wafanyakazi kwa 23.3% ambapo Serikali ilitumia kiasi cha Trilioni 9.7 kwa Mwaka 2022/23 kwa ajili ya kugharamia malipo ya mishahara ya Watumishi wote wa umma kutoka Serikali Kuu, Serikali za Mitaa, Taasisi na Wakala za Serikali, ikiwa ni ongezeko la Trilioni 1.59.


Hatua hii sio tu imekata kiu ya miaka zaidi ya 6 ya Wafanyakazi kutoongezewa mishahara lakini zaidi ni hatua iliyovunja rekodi ya kiwango kikubwa zaidi cha nyongeza ya mishahara kufanyika kipindi hiki ambacho Mataifa mengi Duniani bado uchumi wake umeendelea kustruggle kutokana na janga la Uviko-19, hivyo Serikali iliamua kujibana na kujilipua licha ya changamoto zote za uchumi lakini Wafanyakazi wapate haki yao.


Hatua hiyo iliweka rekodi pia ya ongezeko kubwa la mishahara ukanda mzima wa Afrika Mashariki na Mataifa majirani zetu. Mfano, Kenya waliongeza mishahara kwa 12% tu, Uganda chini ya 10% na Majirani zetu wote kuanzia Rwanda, Burundi, Zambia wao waliongeza chini ya 10% na Mataifa mengine mengi tu kama Sudan Kusini, Congo na mengine yakiwa hata hayajatangaza nyongeza ya mishahara lakini Serikali ya Rais Samia ikipiga 23.3% nyongeza ya mishahara licha ya changamoto zote za uchumi nilizozisema zinazotokana na Uviko-19 na hiyo Vita ya Urusi na Ukraine.


Kama nilivyoandika mara kadhaa, ni ukweli ulio wazi kwamba, changamoto za Wafanyakazi ni zaidi ya kuongezewa mishahara na ni suala lililo wazi kwamba kuongeza mishahara ya Wafanyakazi bila ya kutatua changamoto mbalimbali kwenye mishahara yao na mifumo ya Utumishi ni kazi bure. Ili kumsaidia mfanyakazi, suala la kuongeza mishahara pekee yake halitoshi bila ya kuangalia na kutatua kero zinazosemwa kila kukicha zinazodhoofisha Pato ghafi la mshahara wa Mtumishi.


Toka iingie madarakani, Serikali ya Rais Samia imetupia jicho kutatua kero nyingi za Wafanyakazi ambazo zimekuwa zikila na kupunguza kwa kiwango kikubwa mishahara yao ikiwemo kodi kubwa ya kwenye mishahara, tozo ya mkopo wa Serikali kwa Wafanyakazi wenye madeni ya mkopo wa Elimu ya Juu, malimbikizo ya mishahara na kuajiri Wafanyakazi wapya ili kupunguza mzigo mkubwa kwa Wafanyakazi na changamoto nyingine nyingi. 


Kwahiyo, Serikali ya Rais Samia toka iingie madarakani Machi 19, 2021, si tu amefanya kufuru hii ya nyongeza kubwa ya mishahara iliyovunja rekodi kwa asilimia 23.3 lakini zaidi Serikali yake imeweka nguvu kubwa kutatua kero za Wafanyakazi zinazofanya vipato na mishahara yao kuliwa sana ikiwemo kushusha kodi ya (PAYE)-pay as you earn Kwa asilimia 1 kutoka 9 hadi 8 na hivyo kuongeza moja kwa moja mshahara wa mtumishi ambapo Fedha zilizokuwa zinakatwa kwenye mshahara wa Mtumishi zilipungua.


Eneo hili la PAYE pekee, Serikali ilisamehe kiasi cha Bilioni 14 na Milioni 178 zilizokuwa zinakatwa kwenye mishahara ya Wafanyakazi. Unaona moja kwa moja mshahara wa Mtumishi uliimarika moja kwa moja.


Pia katika kipindi hiki cha uongozi wa Rais Samia, alitatua kero kubwa na ya miaka kwa miaka ya kulipa malimbikizo ya mishahara ya watumishi yenye thamani ya Bilioni 60 na kufanya mabadiliko ya Utumishi yaliyogharimu takribani Bilioni 120. Hapa Serikali ililipa malimbikizo ya mishahara kwa Wafanyakazi 75,000 ambapo Serikali ilitumia Bilioni 124.3


Kufuta ada ya Retention Fee ya asilimia 6 Kwa watumishi wote wenye mikopo ya Elimu ya Juu pamoja na tozo ya adhabu ya asilimia 10 ambayo walikuwa wanakatwa Wafanyakazi wenye Mikopo ya Bodi ya Mikopo ya wanafunzi wa Elimu ya Juu Kwa mwaka kwa ambao walichelewa kulipa na ambao bado hawajamaliza mikopo hiyo na badala ya kulipa fidia kwa kulipa mikopo hiyo, makato hayo yameondolewa.


Kutoa ajira zaidi ya 50,000 mpaka sasa ikiwemo ajira kwenye sekta ya afya, elimu, kwenye vyombo vya ulinzi na usalama, TAKUKURU, Shirika la Reli pamoja na ajira zingine 32,000 zilizotolewa na Serikali mwaka Jana pamoja na hizi 21,200 zilizotangazwa hivi sasa. 


Pia, Serikali ilipandisha vyeo na madaraja Watumishi 85,000 hadi 91,000 mpaka 198,215. Hatua hizi zote za kutoa ajira mpya na kupandisha vyeo na madaraja ni neema tupu maana ilipunguza mzigo mkubwa sana kwa Wafanyakazi.


Unaweza kuona, licha ya nyongeza hii kubwa ya mishahara na kurudisha utaratibu wa nyongeza ya mishahara kila mwaka, lakini Serikali ya Rais Samia imefanya makubwa zaidi kutatua changamoto za Wafanyakazi zilizokuwa zinakula sana mishahara yao, hivyo ongezeko hili la mishahara ni neema kwa ukuaji wa Uchumi wetu na linakwenda kuchochea shughuli za biashara na mzunguko wa fedha nchi nzima maana litaongeza ununuzi, mzunguko wa fedha mtaani na hivyo kuchochea maendeleo ya watu na shughuli zote za uchumi. Historia inaandikwa Tanzania chini ya Rais Samia na kwa kufuru hii, si dhambi kunena kwa madaha kabisa kwamba, Rais Samia ni Kinara wa maslahi ya Watumishi na mjenga Uchumi wa Taifa.

Maoni